Wapendwa kaka na dada zangu,
1. Tangu mwanzo wa utume wangu, nilipenda kuiweka kazi yangu ya
Kipapa chini ya ulinzi maalumu wa Bikira Maria. Nimekuwa daima nikialika
jumuiya yote ya waumini duniani kuishi ile hali waliyoishi wafuasi
katika chumba "cha juu", ambako "waliishi katika
sala pamoja na Maria, Mama wa Yesu" (Mdo 1:14). Katika hati
yangu ya kwanza ya kipapa 'Redemptor hominis' (Wokovu wa watu wote),
niliandika kwamba ni katika hali ya sala ya kina tu, tunaweza kupokea
'Roho Mtakatifu anayetujia na ndipo tunapokea ushuhuda wa Yesu Kristo
hadi miisho ya dunia, kama wale waliokwenda kutoka kile chumba cha
juu hadi Yerusalemu katika siku ya Pentekoste" (n. 22).
Kanisa linazidi kujitambua kuwa ni "Mama" kama alivyo
Maria. Kama nilivyoonyesha wazi katika hati muujiza wa kujifanya
mtu, katika kipindi cha kusheherekea Jubilei Kuu ya mwaka 2000,
Kanisa ni hori ambapo Maria anamweka Yesu ili kumwonyesha awe kiini
cha ibada na tafakari kwa watu wote. (N. 11). Kanisa linaamua kuendelea
na njia hii ya kiroho na umisionari, likisindikizwa na Bikira Maria,
Nyota wa Uinjilishaji mpya, kama taa na msaada wa uhakika katika
hatua kwa hatua (cf. Novo Millenio Ineunte n. 58)
2. MARIA NA UMISIONARI WA KANISA KATIKA MWAKA WA ROSARI
Mwaka jana mwezi Oktoba, katika mwaka wangu wa 25 katika kazi
yangu ya utume wa Petro, nilitangaza kuwa mwaka maalumu, kama
mwendelezo wa roho ile ya Mwaka wa Jubilei, uwe ni mwaka wa kutafakari
na kugundua zaidi juu ya sala ya Rozari, sala muhimu sana katika
Utamaduni wa Kikristo! Ni mwaka tunaopaswa kuishi kwa kumfuata
mmoja ambaye kwa mpango wa Mungu, pamoja na jibu lake la "Ndiyo",
amewezesha wakovu kwa watu wote utendeke, na anaendelea kutoka
mbinguni kuwalinda wale wote wanaomkimbilia, hasa wakati wa shida
mbalimbali katika maisha yao.
Ningependa mwaka huu wa Rozari uwe muda mwafaka kwa waumini katika
makontinenti yote, kuingia kwa undani zaidi ili kuelewa vema maana
ya wito wao wa Ukristo. Kwa njia ya shule hii ya Bikira Maria
na kwa mfano wa maisha yake, ni vyema kwamba kila jumuiya itatokea
kwa vizuri zaidi kuwa na namna itakayoiwezesha kutafakari na kuingia
zaidi katika Umisionari.
Iwapo Jumapili ya Uenezaji wa Injili, ambayo itafikia siku za
mwisho za mwaka umaalumu wa Maria, itaandaliwa vizuri, italeta
kiu kubwa ya moyo wa kujituma katika jumuiya ya kanisa. Makimbilio
yetu kwa Bikira Maria, pamoja na kusali Rozari kila siku na pia
kutafakari mafumbo ya maisha ya Kristo, yatahamasisha kuwa kazi
ya Kanisa lazima itegemezwe kwanza kabisa kwa njia ya sala. Tabia
ya "kusikiliza", ambayo inafanywa kwa njia ya kusali
Rozari, inampeleka waumini awe karibu sana na Bikira Maria, ambaye
"aliyaweka mambo yote haya, akiyatafakari moyoni mwake".
(Lk. 1:19). Tendo la kutafakari mara kwa mara Neno la Mungu hutufanya
tuishi, "Katika umoja na Yesu kwa njia (twaweza kusema) ya
moyo wa Mama peke yake" (Rozarium Virginis).
3. KANISA LINALOTAFAKARI ZAIDI: SURA YA KRISTO
ALIYETAFAKARIWA:
Cum Mariae Contemplemur Christ Vultum!
Maneno haya hunijia mara nyingi akilini. Tafakari "Sura"
ya Kristo pamoja na Maria. Tunapozungumzia "Sura" ya
Kristo, tunazungumzia juu ya kufanana kwake na binadamu, ambapo
utukufu wa milele wa mwana pekee wa Baba unang'ara juu yake (angalia
Yoh. 1:14): "Utukufu wa Mungu kama kichwa unang'ara kutoka
katika Sura ya Kristo". (RVM - 21). Kuitafakari Sura ya Kristo
kunapelekea katika undani wa kina, undani wa kidugu katika fumbo
lake. Kumtafakari Yesu kwa macho ya imani kunamfanya mtu apenye
hadi katika fumbo la Utatu Mtakatifu wa Mungu. Yesu anasema. "Yeye
aliyeniona mimi amemwona Baba." (Yoh. 14:9). Kwa njia ya
Rozari tunasonga mbele zaidi katika safari ya fumbo hili, "pamoja
na katika shule ya Mtakatifu sana Mama yake, (RVM - 3). Hakika,
Maria anajifanya yeye mwenyewe kuwa mwalimu na mlinzi wetu.
Kwa njia ya Roho Mtakatifu anatusaidia tuwe na huo utulivu katika
ulinzi huo unaowafanya waumini wasambaze imani yao kwa njia ya
uzoefu wao katika Yesu na kwamba ni tumaini linalowahamasisha
(RM - 24). Tumwone daima Maria, kama modeli asiye na mfano wa
kulinganishwa. Maandiko yote ya Injili yanapata umaana usio kifani
katika nafsi yake.
Bikira Maria ni kumbukumbu ya tafakari ya Kanisa liishilo na
hamu ya kuunganika katika undani wake na Bibi harusi wake, ili
kuwa na uhusiano wa ndani zaidi katika jamii yetu.
Je, tunajimudu vipi katika matatizo makubwa, katika mateso yasiyo
ya haki, ukosefu wa haki aliingia kwa kiburi? Katika shule tulivu
ya Maria Mama yetu, waumini wanajifunza kumtambua katika "ukimya
wa Mungu unaojitokeza", Neno anayetenda katika ukimya kwa
ajili ya wokovu wetu.
4. Kwa njia ya Ubatizo waumini wote wanaalikwa kwenye Utakatifu.
Katika kanuni ya mwongozo 'Lumen Gentium', Mtaguso Mkuu wa II
unasisitiza kuwa wito huo kwa jumla unatokana na wito wa wote
kuelekea ukamilifu wa upendo.
Utakatifu na Umisionari ni maswala yasiyoweza kutenganishwa kuhusu
wito wa kila mbatizwa. Hali ya kujitoa na kuwa Mtakatifu zaidi
inaenda sambamba na ile ya kutawanya ujumbe wa wokovu. Katika
Redemptoris Missio, nilikumbusha kuwa "Kila mmoja katika
jumuiya ya waumini anaalikwa kwenye Utakatifu na Umisionari".
(N.90). Katika kutafakari mafumbo ya Rozari, muumini anahamasishwa
kumfuata Kristo na kushirikisha maisha yake, hivyo anaweza kuyarudia
maneno ya Mtakatifu Paulo yasemayo "Siyo mimi niishiye bali
ni Kristo aishiye ndani mwangu" (Gal. 2:20).
Iwapo mafumbo ya Rozari yanaunda shule muhimu ya kuelekea Utakatifu
na Uinjilishaji, basi Mafumbo ya Mwanga yanarahisisha kwa namna
fulani juu ya kuielewa vyema Injili, "Sequela".
Ubatizo wa Yesu katika mto Yordani unatukumbusha kwamba waliobatizwa,
wameteuliwa kuwa "Waana wa Mwana" (Ef. 1:5; Gaudium
et Spe N. 22).
Katika harusi ya Cana, Maria anawaalika wafuasi kumsikiliza kwa
utii Neno wa Bwana: "Fanyeni lolote analowaambia" (Yoh.
2:5). Kutangazwa kwa Ufalme wa Mungu na waliko wa kutubu ni alama
wazi ya Utume wa kila mmoja kuelekea Utakatifu.
Katika kubadilika Sura kwa Yesu, mbatizwa anaonja furaha inayomngoja
baadaye. Katika kutafakari kuwekwa kwa Ekaristi Takatifu, mbatizwa
anarudishwa kila mara katika "Chumba cha Juu", ambako
Bwana aliwaachia Mitume wake utajiri mkuu kuliko wote: Yeye mwenyewe
katika Sakramenti ya Altare. Kwa namna nyingine, ni yale maneno
ambayo Bikira Maria aliyatamka pale Cana ndiyo yanajenga kumbukumbu
ya Bikira Maria katika mafumbo yote ya Mwanga.
Hakika kumtangazwa kuwa Ufalme wa Mungu umefika, mwaliko kwa
toba na huruma, kubadilika Sura mlimani Tabor na kuwekwa kwa Ekaristi
Takatifu yanapata mwangwi maalumu katika Moyo wa Bikira Maria.
Maria anayaelekeza macho yake kwa Kristo, anahifadhi kila neno,
anatuonyesha jinsi ya kuwa wanafunzi halisi wa Mwanae.
5. KANISA LA KIMISIONARI ZAIDI: KUTANGAZWA KWA SURA YA KRISTO:
Haijawahi kutokea Kanisa likawa namna nyingi za kumtangaza Yesu
kama sasa, shukrani nyingi kwa maendeleo ya teknolojia ya vyombo
vya mawasiliano katika jamii. Kwa maana hiyo Kanisa la leo linaalikwa
kuhakikisha kuwa Sura ya bibi harusi (Kanisa) inang'ara na kupendeza
zaidi katika Utakatifu wake. Katika hili, kwa urahisi tu Kanisa
linajua kuwa linasimamiwa na Mama Maria. Kwa njia ya Maria, "Linajifunza"
kuwa "Bikira", anayejitoa kikamilifu kwa Bwana harusi
wake, Yesu Kristo, na kwamba "Mama" wa watoto wengi
ambao anawaelekeza kwenye uzima wa milele.
Chini ya uangalifu mkubwa wa Mama yake, jumuiya ya kanisa inashamiri
kama familia iliyoimarishwa na mmiminiko mkubwa wa nguvu ya Roho,
na inayopokea na kukubali mapokeo mapya ya Unjilishaji, inatafakari
sura yenye huruma ya Yesu katika ndugu, hasa katika wale maskini
na wahitaji, katika wale walio nyuma katika imani na elimu ya
Injili. Kwa namna ya pekee, Kanisa haliogopi kuuhubiria ulimwengu
kwa nguvu zote kuwa Kristo "ni njia, ukweli na Uhai"
(Yoh. 14:6). Haliogopi kutangaza kwa furaha kuhusu "Habari
njema, yenye nafsi Yesu Kristo kama kiini na roho, Neno aliyefanywa
mwili, mkombozi pekee wa ulimwengu" (Rosarium Virginis Mariae
- N. 20).
Ni vyema kuwaandaa wainjilishaji wenye uwezo wa walio wa Watakatifu.
Utendaji wa roho ya mitume unatakiwa usipungue nguvu hata kidogo
hasa katika swala la Utume kwa watu (umisionari ad gentes). Rozari
ikigundulika vizuri na kupendwa ni namna tena ya kawaida izaayo
matunda mema katika kuelimisha na ni chombo cha kiroho kwa ajili
ya kuwafanya Taifa la Mungu kufanya kazi katika uwanja mpana katika
shughuli za Kichungaji.
6. UTUME (MAHSUSI)
Kazi ya uongozi wa kimisonari lazima uendelee kuwa mathubuti,
wajibu dhahiri kwa kila mbatizwa na jumuiya yoyote ya Kanisa.
Mashirika ya Kipapa ya Kimisionari, ni wazi yana kazi dhahiri
na ya pekee, na ninayashukuru kwa kutenda jukumu hilo kwa ukarimu
wote. Napenda kutoa wazo kwenu nyote kwamba iwapo jitahidini kuimarisha
sala ya Rozari, binafsi na katika jumuiya, ili kupata kutoka kwa
Bwana zile neema ambazo Kanisa na wanadamu wote kwa kweli wanahitaji.
Namwaalika kila mmoja kufanya hivyo: Watoto, watu wazima, vijana
na wazee, familia, maparokia na jumuiya za watawa.
Kati ya nia nyingi singependa kusahau ile ya kuomba Amani. Vita
na hujuma vina kiini chake katika moyo "aliogawanyika."
Kila mmoja anayetafakari juu ya fumbo la Kristo - na hii ni dhahiri
lengo la Rozari - hujifunza siri ya Amani na anaifanya kuwa ni
mradi wake. (RVM - N. 40).
Iwapo Rozari inajenga amani katika kasi ya maisha yetu, kinaweza
kuwa ni chombo mahsusi kilichopendelewa kwa ajili ya kujenga amani
ndani ya mioyo ya watu. Katika familia na kati ya watu. Pamoja
na Maria, tunaweza kupata chochote tuombacho kutoka kwa mwanae
Yesu. Kwa msaada wa Maria, hatutasita kujitoa kwa ukarimu katika
kutangaza Habari Njema hadi miisho ya dunia.
Katika mawazo haya, kwa upendo mkubwa nawabariki nyote.
Imetolewa:
Vatican, 12 Januari, 2003
Sikukuu ya Ubatizo wa Bwana.
IOANNES PAULUS II
|